Matangazo yanakaribishwa katika blog hii,piga simu no 0753 239 687 Email-livinusferuzi@yahoo.com

Friday, October 26, 2012

MVUA KUBWA ZALETA MADHARA KAGERA



  .
Miongoni mwa nyumba zilizoezuliwa na mvua iliyoambatana na upepo mkali katika kata ya  Buhembe nje kidogo ya mji wa  Bukoba.

Na mwandishi wetu
Bukoba

NYUMBA zilizoezuliwa na mvua iliyoambatana na upepo mkali (Oktoba 25) katika manispaa ya Bukoba zimeongezeka kutoka nyumba 25 hadi kufikia nyumba 93 na kupelekea wananchi 436 kuachwa bila makazi.

 Mvua hiyo iliyonyesha jana asubuhi kwa takribani nusu saa ilipelekea kuezuliwa kwa nyumba hizo, huku baadhi yake kubomoka kwenye kata tatu za Buhembe, Kahororo na Nyanga, ambapo pia imeharibu mazao mbalimbali na kusababisha hofu ya njaa kwa wananchi husika.

Diwani wa kata ya Buhembe Bw. Alexander Ngalinda alisema kuwa katika kata yake nyumba 68 zimeezuliwa na kusababisha wananchi wanaokadiriwa kufikia 340 kukosa mahala pa kuishi.

Bw. Ngalinda alitaja mazao yaliyoharibiwa na mvua hizo kuwa ni pamoja na mahindi, maharage, migomba na marando, ambapo tathimini ya hasara iliyosababishwa na maafa hayo bado inaendelea kufanyika.

Katika Kata ya Nyanga nyumba 15 zimeezuliwa na baadhi yake kubomoka ambapo wananchi wanaokadiriwa kufikia 60 wamalazimika kulala kwa majirani baada ya kukosa mahali pa kulala .

Naye Diwani wa kata ya Nyanga Bw. Deusdedith Mtakyahwa alisema kuwa bado wanaendelea kutembelea maeneo yote ya kata hiyo ili kubaini athari nyingine zilizotokana na mvua hizo.

Mwenyekiti wa mtaa wa Bunukangoma uliopo kata Kahororo, ambayo ni kata nyingine iliyoathiriwa na mvua hizo Bw, Cosmas Rwabigene alisema kuwa katika mtaa wake wananchi 36 hawana makazi kufuatia nyumba zao kumi kuathiriwa na mvua hizo.

Wananchi katika kata hizo zilizoathirika wameomba serikali na wadau wengine kuwasaidia fedha za kununulia mabati na kujengea nyumba zao na ikiwa ni pamoja na kupatiwa chakula kufuatia mazao waliyoyategemea kuharibika.

Mkuu wa mkoa wa Kagera kanali mstaafu Fabian Massawe ameanza ziara rasmi katika kata zilizoathirika ili kujionea hali halisi na tathmini ya harasa iliyosababishwa na mvua hizo itatolewa baadae.

Mwisho.


No comments:

Post a Comment