Matangazo yanakaribishwa katika blog hii,piga simu no 0753 239 687 Email-livinusferuzi@yahoo.com

Monday, June 25, 2012

WAKULIMA WA KAHAWA WAGOMA KUWAUZIA KAHAWA KCU

Mwenyekiti wa bodi ya chama cha ushirika mkoa wa Kagera KCU Bw. John Binushu akifungua mkutano mkuu wa chama hicho, mkutano huu ndio ulitangaza bei ya kahawa kwa msimu huu

Baadhi ya wajumbe wa mkutano mkuu, ambao ndio wawakilishi wa wakulima wakifuatilia mkutano ambao ulitangaza bei ya kahawa

Na Livinus Feruzi
Bukoba

WAKULIMA wa zao la kahawa mkoa wa Kagera wamepinga vikali kitendo cha chama kikuu cha ushirika mkoa wa Kagera (KCU 1990 LTD) kushusha bei ya zao hilo tofauti na iliyotangazwa awali katika mkutano mkuu wa makisio, huku wakisisitiza kuwa hawako tayari kuuza chini ya bei ya awali.

Wakulima hao walitoa msimamo huo jana kwa nyakati tofauti wakati wakizungumza na waandishi wa habari, ambapo walisema katika mkutano huo walitangaziwa bei itakayotumika kununulia kahawa katika msimu huu, na kuwa kwa sasa wanashangaa kuona wanapelekewa barua ya kupunguzwa kwa bei hiyo.

Kwa mujibu wa wakulima hao maandalizi ya kahawa yanachukua muda mrefu ikia ni pamoja na kutumia gharama kubwa katika kuandaa kahawa, huku wakiweka wazi msimamo wao wa kutokubaliana na sababu zozote za kupunguza bei ya zao hilo, ambalo ndio tegemeo kwa wakulima wa mkoa wa Kagera.

Mmoja wa wakulima hao Bw. Burchard Laurent alisema kuwa bei iliyotangazwa  awali ilikuwa  nafuu kwa mkulima ambayo kwa kiasi fulani alidai ingesaidia kuwapunguzia makali ya maisha yanayowakabili wakulima.

Alisema kauli ya KCU ya kuwa tatizo hilo la kushusha bei linatokana na kushuka kwa bei ya kahawa katika soko la dunia sio kweli kwani hata makapuni binafsi yanayonunua kahawa ya wakulima kwa bei pia yangetangaza kushusha bei.

“Kama KCU wataendelea kug’ang’ania kununua kahawa kwa bei ya punguzo wakulima hawatawauzia kahawa yao na badala yake watawauzia wanunuzi na makampuni binafsi ambao mpaka sasa wao bado wananunua kwa bei nzuri” alisisitiza Bw. Laurent

 Awali  KCU ilitangaza bei ya kununulia kahawa ya wakulima ambapo kwa msimu wa 2012/2013  kahawa aina ya Robusta maganda ilitangazwa kununuliwa kwa shilingi 1,360  kwa kilo huku Arabica maganda ikitangazwa kununuliwa kwa shilingi 1,550.

Kwa upande wa Robusta safi ilitangazwa kununuliwa kwa  shilingi 2,700 kwa kilo na  shilingi 3,200 kwa Arabica safi, huku kahawa ya Arabica  organic iliyotangazwa ilikuwa shilingi 3,800, Robusta ya Organic shilingi shilingi 3,650 na Robusta Organic ya Uganda shilingi 1,700.

Hata hivyo Kwa mujibu wa barua iliyoandikwa Juni 19 mwaka 2012 na kusainiwa na meneja mkuu wa  KCU Bw. Vedasto Ngaiza na kusambazwa katika vyama vyote vya ushirika vya msingi, bei ya kahawa inapungua tofauti na iliyotangazwa awali kwa madai ya kushuka kwa bei ya zao hilo  soko la dunia.

Barua hiyo majiwa imepata nakala inasema kahawa ya robusta ya maganda imepungua kutoka shilingi 1,360 hadi shilingi 1,100 kwa kilo moja, ambapo robusta safi imepungua kutoka shilingi 2,700 hadi shilingi 2,200.

Aidha barua hiyo inasema kuwa kahawa aina ya Arabica maganda imepungua kutoka shilingi 1,550 hadi shilingi 1,300 huku Arabica safi itapungua kutoka shilingi 3,200 awali hadi shilingi 2,600.

 Hata hivyo katika barua hiyo Meneja mkuu huyo wa KCU Bw. Ngaiza anasema bei ya kahawa aina ya Robusta kwenye soko la dunia ndio imeshuka, huku akiwa haonyeshi sababu za kupelekea KCU kushusha kahawa aina ya Arabica .

mwisho

No comments:

Post a Comment